Leading Centre of Excellence for Knowledge, Skills, and Applied Education in Science and Technology
MUST KUENDELEA KUTOA FURSA YA ELIMU KWA WAFANYAKAZI WAKE
Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya (MUST) kitaendelea kutoa fursa ya elimu kwa Wafanyakazi wake watakaotaka kwenda masomoni.
Hayo yamesemwa mapema leo na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya Prof. Aloys Mvuma katika Mkutano wa Wafanyakazi uliofanyika katika Ukumbi wa Nyerere uliopo Chuoni hapo.
Prof. Mvuma amesema kuwa Chuo kitaendelea kutoa fursa kwa Wafanyakazi kwenda masomoni bila kikwazo chochote ili kuwapa fursa kuongeza kiwango cha elimu walichonacho.
Amesema kuwa hadi sasa idadi ya Wafanyakazi ambao wapo masomoni ni 173 na kuwa wataendelea kutoa fursa zaidi kwa Wafanyakazi watakaotaka kujiendeleza.
Amesisistiza Wafanyakazi wa Kada ya Taaluma kujikita zaidi katika kufanya machapisho na tafiti ambapo amepongeza jitihada zinazofanywa na Wahadhiri wa Chuo hiko katika kuandaa machapisho na tafiti.
Sambamba na hilo amesema kuwa Chuo kitaendelea kuboresha maslahi ya Wafanyakazi, mazingira ya kufanyia kazi pamoja na ya kufundishia ili kuongeza ufanisi katika kazi.
Aidha amewataka Wafanyakazi kufanya kazi kwa ushirikiano bila kuweka matabaka ili kuhakikisha malengo yote muhimu ya Taasisi yanatimia.
Nao Viongozi wa Vyama vya Wafanyakazi Chuoni hapo Bw. Emmanuel Mwangomo na Dr. Daniel Sinkonde wamepongeza uongozi wa Chuo kwa kuwaleta Wafanyakazi pamoja bila kujali vyama wanavyotoka ili kujadili mafanikio,changamoto na malengo ya kazi kwa mwaka unaofuata.
Aidha katika Mkutano huo Mkuu wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu Bi. Judith Egina aliainisha Wafanyakazi bora kwa mwaka 2021/2022 na kukabidhiwa vyeti ili kutambua mchango wao.
Mkutano huo ni muendelezo wa Mikutano inayofanyika mara kwa mara Chuoni hapo yenye lengo la kutoa taarifa ya mafanikio mbalimbali ya Taasisi, mwelekeo wa Taasisi na kuwaunganisha pamoja menejimenti na Wafanyakazi ili kufanya maamuzi ya wazi kwa pamoja kama Taasisi.